Mapema leo tarehe 23 Februari 2024 Mkuu wa Wilaya ya Mbinga Mhe. Aziza Mangosongo ametembelea Kituo cha Afya Kindimbachini kuwajulia hali wanafunzi 11 ambao wamejeruhiwa na radi tarehe 22 Februari 2024.
Sambamba na kuwatembelea majeruhi hao Mangosongo ameshiriki mazishi ya wanafunzi Maria Hyera(10) Alfons Hyera (8) kutoka shule ya msingi Mapendano pamoja na Deus Kayombo ( 8) kutoka Shule ya Msingi Kindimbachini ambao wamepoteza maisha kutokana na radi hiyo.
Aidha amekabidhi majeneza matatu na rambirambi kwa wazazi wa marehemu pamoja na pole kwa majeruhi ambao wanaendelea kupata matibabu katika kituo cha Afya Kindimbachini.
Ili kuhakikisha afya za majeruhi hao zinaimarika Mangosongo amemuagiza Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kindimbachini kuwa huduma za afya kwa majeruhi hao zitolewe bure kwa kuzingatia ubora zaidi.
Akitoa salamu za pole Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Andrew Mbunda amemhakikishia Mkuu wa Wilaya kuwa huduma za afya zitatolewa kwa ubora kama alivyoagiza.
Naye Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kindimbachini Dkt. Salum Bundala amebainisha kuwa kutoka na kadhia hiyo wanafunzi 3 wamepoteza maisha, na wanafunzi 20 walijeruhiwa na kufikishwa kituoni hapo kwa ajili ya kupatiwa matibabu ambapo kati yao 9 wameruhusiwa na 11 wanaendelea na matibabu na hali zao zinaimarika.
Akielezea tukio kwa upande wa shule ya Msingi Mapendano Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Danstan Hyera amebainisha kuwa majira ya saa tisa alasiri radi ilipiga na wanafunzi 21 walidhurika kati yao 19 walijeruhiwa na wanafunzi 2 walipoteza maisha.
Kwa upande wake Bi. Anna Mkifaru ambae ni mzazi wa moja ya majeruhi amewashukuru watoa huduma wa Kituo cha Afya Kindimbachini kwa huduma bora zinazoendelea kutolewa kwa majeruhi hao ambao afya zao zinaendelea kuimarika.
Jumla ya Wanafunzi waliokubwa na kadhia hiyo ni 23, wanafunzi 2 kutoka shule ya msingi Kindimbachini na wanafunzi 21 kutoka Shule ya msingi Mapendano shule zilizopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga.
Imeandikwa na Silvia Ernest
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
23 Februari 2024
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit