Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga inatarajia kutekeleza mradi mkubwa wa Kuboresha Miliki za Ardhi kwenye vijiji 50 kati ya 117 vya Halmashauri hiyo kuanzia mwaka huu wa fedha 2022/2023.
Katika Kikao cha kutambulisha mradi kilichoongozwa na Maafisa wa Wizara ya Ardhi leo Jumatano Januari 11, 2023 katika Ofisi za Halmashauri Kiamili na kukutanisha pia Maafisa kutoka Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Mkoa wa Ruvuma, Maafisa Ardhi, Wakuu wa Idara na Vitengo na Timu ya Utekelezaji wa mradi ngazi ya Halmashauri, Meneja wa Mradi Taifa Bw. Joseph John Osena amesema Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ni miongoni mwa Halmashauri 41 za mfano zitakazoanza utekelezaji wa mradi huo wa miaka mitano kati ya Halmashauri zote 184 nchini.
Bw. Osena amefafanua kuwa pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ambayo ni Halmashauri pekee ya mfano kwa Mkoa wa Ruvuma katika awamu hii ya kwanza ya utekelezaji wa mradi kuna Halmashauri nyingine 40 kutoka Mikoa ya Arusha, Pwani, Simiyu, Tanga, Tabora, Geita, Kigoma, Mara, Shinyanga, Dodoma, Iringa, Mbeya, Kilimanjaro, Songwe na Katavi na kwamba katika utekelezaji wake katika Halmashauri hizo Serikali inakusudia kuandaa, kumilikisha na kugawa jumla ya Hatimiliki za Ardhi (CROs) na Leseni za Makazi Milioni 2 kwenye maeneo ya mijini na Hatimiliki za Kimila (CCROs) 500,000 kwa maeneo ya vijijini.
Kwa upande wake Mratibu wa mradi ngazi ya Halmashauri Bw. Maurus Hyera amesema kupitia mradi huo shughuli mbalimbali zinatarajiwa kuanza utekelezaji wake hivi karibuni ambazo zitahusisha uboreshaji wa Ofisi za Baraza la Ardhi la Wilaya, uboreshaji wa masijala za ardhi za vijiji, pamoja na uandaaji wa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi (Land Use Plans) ngazi ya Wilaya lakini pia kwenye vijiji vyote 50 vya mradi.
Vilevile mradi utahusisha zoezi la upimaji wa mipaka ya vijiji utaoambatana na uandaaji na ugawaji wa Vyeti vya Ardhi kwa kila kijiji cha mradi lakini pia kushughulikia suala la usalama katika umiliki wa ardhi ambapo zaidi ya Hatimiliki za Kimila 40,000 zitaandaliwa na kugawiwa kwa wananchi.
Imeandikwa na
Salum Said
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Tarehe 11 Januari, 2023
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit