Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Juma Haji Juma amekabidhi vyumba 10 vya madarasa yenye thamani ya shilingi Milioni 200 kwa Mkuu wa Wilaya ya Mbinga katika hafla iliyofanyika Shule ya Sekondari ya Wasichana Mbinga eneo la Kiamili, Kata ya Kigonsera Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma.
Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi mbele ya Mkuu wa Wilaya ya Mbinga wakati wa hafla hiyo leo Januari 6, 2023 Mkurugenzi Mtendaji amesema fedha za ujenzi wa madarasa hayo 10 ambayo yamejengwa kwenye Shule 5 za Sekondari za Kipapa, Kipololo, Litumbandyosi, Mahilo na Mbinga Girls zimetolewa na Serikali Kuu.
Ameongeza kuwa ujenzi wa madarasa hayo ulioanza tarehe 20 Oktoba 2022 mara baada ya mapokezi ya fedha ulikamilika tarehe 15 Disemba 2022, utekelezaji wake ukijumuisha pia uwekaji wa samani yaani meza na viti kwenye kila chumba cha darasa.
Akizungumza mara baada ya kukagua na kupokea taarifa ya mradi, Mkuu wa Wilaya ya Mbinga Mhe. Aziza Mangosongo amempongeza Mkurugenzi na watendaji wa Halmashauri kwa usimamizi mzuri katika utekelezaji wa mradi na kwamba yeye mwenyewe binafsi amejionea namna madarasa hayo pamoja na samani zake yalivyojengwa kwa viwango na ubora unaostahili huku akielekeza walimu kusimamia utunzaji wa miundombinu hiyo kwenye shule zao.
Aidha Mhe. Mangosomo ametoa wito kwa jamii kuchangamkia zoezi la uandikishaji wa wanafunzi wa darasa la kwanza na elimu ya awali kipindi hiki likiwa linaelekea ukingoni na kuhakikisha wanachangia nguvu zao ili kuunga mkono jitihada za serikali katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye maeneo yao.
Naye Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini Mhe. Benaya Kapinga amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali yake kwa kuipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga fedha nyingi na kuiwezesha kutelekeza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo Jengo la Utawala na Ofisi za Halmashauri, Hospitali, Nyumba ya Mkurugenzi na Wakuu wa Idara pamoja na madarasa hayo ambayo yamekabidhiwa kwa Mkuu wa Wilaya tayari kwa kuanza kutumiwa na wanafunzi mara tu shule zitakapofunguliwa.
Imeandikwa na
Salum Said
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga
Tarehe 6 Januari, 2023
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit