Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. David Silinde ameridhishwa na ubora wa madarasa yanayoyengwa kwenye maeneo mbalimbali wilayani Mbinga huku akipongeza kasi nzuri ya utekelezaji wa miradi hiyo.
Hayo yamejiri disemba 17, 2021 wakati wa ziara ya Naibu Waziri huyo alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa vyumba vya madarasa yanayojengwa kwenye maeneo mbalimbali ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19.
Mhe. Silinde amesema ameridhishwa na thamani, ubora na kasi ya utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga na Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla na kwamba lengo la serikali ni kuona madarasa yote yanayojengwa nchini kupitia mpango huu yanakamilika kwa wakati na kwamba ifikapo Januari 2022 wanafunzi wote 907,802 waliochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza wanaanza masomo yao mara moja.
“Kwa ujumla Mkoa wa Ruvuma upo mbele zaidi ukilinganisha na maeneo mengi; Rais anataka mwakani 2022 madarasa na madawati ndio yawasubiri wanafunzi, na sio kinyume chake”. Amesisitiza Mhe. Silinde
Naibu Waziri wa TAMISEMI Mhe. David Silinde amefanya ziara yake Wilayani Mbinga akitokea Wilaya ya Songea ambapo ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa vyumba vya madarasa kwenye shule za Sekondari za Mkako, Kiamili na Shule ya Sekondari ya Wasichana Mbinga (Mbinga Girls) zilizopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga na Shule za Sekondari za Ruhuwiko na Makita kwa upande wa Halmashauri ya Mji wa Mbinga.
Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ipo kwenye hatua za mwisho za ukamilishaji wa vyumba vya madarasa 88 kwenye shule 30 za sekondari vyenye thamani ya shilingi Bilioni 1.76 ikiwa ni miongoni mwa madarasa 1,200 yanayojengwa kwenye shule za sekondari na madarasa 300 yanayojengwa kwenye shule shikizi kote nchini kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19
Imeandikwa na
Salum Said, Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga
Tarehe 17 Disemba 2021
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit