Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Brig. Jen Wilbert Ibuge ametoa wito kwa wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya masikini TASAF Wilayani Mbinga kutumia fedha za ruzuku zinazotolewa kupitia mpango huo kwa kujikwamua kiuchumi na kujiletea maendeleo.
RC Ibuge ametoa wito huo leo Januari 18, 2022 wakati wa ziara yake katika Kijiji cha Amanimakolo kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ambapo amepokea taarifa ya utekelezaji wa Mpango kwenye Kata ya Amanimakolo na kutembelea kaya za walengwa na wanufaika wa Mpango huo kijijini hapo.
Mhe. Mkuu wa Mkoa amesema wanufaika wanapaswa kutambua na kuthamini uzito wa kile wanachokipokea kupitia TASAF na kwamba fedha hizo zitekeleze na kutumika kama zilivyokusudiwa ikiwemo kugharamia mahitaji ya watoto shuleni na bima ya afya ya jamii iliyoboreshwa (iCHF) huku akipongeza jitihada zilizofanyika kuwezesha asilimia 77 ya kaya zote za wanufaika wa TASAF wilayani Mbinga kujiunga na mfuko huo.
Awali akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini Wilayani Mbinga, Mkuu wa Wilaya hiyo Bi. Aziza Mangosongo amesema kwa kipindi cha mwezi Mei hadi Oktoba 2021 Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ilipokea jumla ya shilingi 908,398,800 kwa ajili ya malipo kwa kaya 8,669 zinazonufaika na Awamu ya Tatu, Kipindi cha Pili cha utekelezaji wa Mpango huo kutoka kwenye vijiji vyote 117 vya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga
Aidha, Mhe. Mangosongo amefafanua malengo ya mpango huo wa TASAF kuwa ni kuziwezesha kaya masikini kuongeza kipato, fursa na uwezo wa kugharamia mahitaji ya msingi kama chakula, afya, malazi, elimu na makazi, sambamba na kupokea ruzuku ya masharti kwa watoto kuhudhuria shule na kliniki.
Akielezea namna wananchi wanavyonufaika na mpango wa TASAF na mafanikio yaliyopatikana kutokana na utekelezaji wake kwenye vijiji vya Amanimakolo, Kiwombi na Mkeke vilivyopo Kata ya Amanimakolo Bw. Joachim Ngaponda ambaye ni Afisa Mtendaji wa Kata hiyo amesema mpango huo umechangia kuongezeka kwa mzunguko wa fedha na msukumo wa shughuli mbalimbali za kiuchumi vijijini, ongezeko na hamasa ya jamii kujiunga na mfuko wa afya ya jamii ulioboreshwa
Bw. Ngaponda ameongeza kuwa mpango huo wa kusuru kaya masikini umechochea kuimarika kwa mahudhurio na kupungua kwa utoro wa vipindi kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari, huku mmoja wa wanufaika wa mpango huo Bi Orenata Markus Haule akieleza kuwa kupitia ruzuku anayopokea kupitia TASAF amefanikiwa kugharamia mahitaji ya shule kama vile sare za shule, viatu na mahitaji mengine jambo ambalo kabla ya mpango lilikua gumu kwa upande wake kutokana na hali duni ya maisha aliyokua nayo.
Imeandikwa na Salum Said
Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga
Tarehe 18 Januari, 2022
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit