Timu ya Viongozi na Wataalamu kutoka Wilaya ya Ludewa Mkoani Njombe imefanya ziara ya kutembelea Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga iliyopo Mkoani Ruvuma kwa lengo la kujionea namna Halmashauri hiyo inavyonufanika kupitia uwekezaji kwenye sekta ya madini aina ya makaa ya mawe.
Ugeni huo ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa Sunday Deogratius aliyembatana na Wataalam ambao ni Mhasibu wa Mapato, Mwanasheria, Mweka Hazina, Afisa Madini Mkoa wa Njombe na viongozi wengine uliwasili mapema Jumatatu Januari 24, 2022 na kufanya mazungumzo na timu ya wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ikiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Juma Haji Juma kwenye Ofisi za Halmashauri zilizopo Kiamili.
Mara baada ya kufanya mazungumzo hayo timu hiyo ya viongozi na wataalam kutoka Wilaya ya Ludewa ilitembelea kituo cha ukaguzi na geti la kukusanyia ushuru la Kitai na kujionea namna ukusanyaji wa mapato na ushuru unaotokana na makaa ya mawe unavyofanyika kupitia kituo hicho kabla ya kutembelea eneo la bandari kavu ya makaa ya mawe ineyoendeshwa na Kampuni ya Ruvuma Coal iliyopo Mkeso ambapo walijionea namna shughuli za uchimbaji, usafirishaji, uchakataji na uuzaji wa makaa ya mawe zinavyofanyika.
Ziara hii ya wataalam na viongozi wa Wilaya ya Ludewa kutembelea Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga kujifunza namna Halmashauri na jamii Wilayani Mbinga inavyonufaika na uwekezaji kwenye sekta ya makaa ya mawe imekuja ikiwa ni mkakati wa mapema wa viongozi hao katika kujipanga kupokea uwekezaji kwenye sekta ya madini ya makaa ya mawe kabla ya kuanza rasmi kwa shughuli za uchimbaji na uchakataji wa madini hayo unaotarajiwa kuanza hivi karibuni Wilayani Ludewa.
Uwekezaji kwenye sekta ya madini ya makaa ya mawe umekua ukifanyika kwa zaidi ya miaka 10 sasa ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ambapo awali Tancoal ndio ilikua kampuni pekee iliyokua ikijishughulisha na uchimbaji wa makaa ya mawe kabla ya kuongezeka kwa makampuni kama Ruvuma Coal, Jitegemee Holdings na wawekezaji wengine na hivyo kuongeza uzalishaji na wigo wa mapato yatokanayo na makaa ya mawe kwa jamii na Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga.
Imeandikwa na
Salum Said, Mbinga
24 Januari, 2022
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit