Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini Mhe. Benaya Kapinga kupitia fedha za Mfuko wa Jimbo amegawa vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya shilingi Milioni 78.6 kwa Madiwani na Watendaji wa Kata 22 kwa ajili ya kwenda kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye maeneo hayo.
Ugawaji wa vifaa hivyo vinavyojumuisha mabati, saruji na nondo umefanyika leo Ijumaa Februari 3, 2023 katika Ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga zilizopo Kiamili zoezi ambali limeongozwa na Mkurugenzi Mtendaji ambaye pia ni Katibu wa Mfuko wa Jimbo Bw. Juma Haji Juma huku Mbunge huyo akiwakilishwa na Katibu wake Ndg. Anton Hyera ambapo pia Mwenyekiti wa Halmashauri Mhe. Desderius Haule, Madiwani, Watendaji wa Kata na watendaji wengine wa Halmashauri wameweza kushuhudia.
Mhe. Denis Kapinga ni mmoja wa Madiwani walionufaika na mgao huo ambaye baada ya kutoa shukrani zake kwa Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini na Serikali kwa ujumla amesema vifaa hivyo vitaenda kukamilisha mradi wa nyumba ya watumishi wa afya (2 in 1) huku Diwani wa Kata ya Wukiro Michael Komba naye pia akibainisha kuwa vifaa hivyo vitaelekezwa kwenye ukarabati wa nyumba ya mwalimu na mradi wa ujenzi wa choo cha kudumu Shule ya Msingi Mkalite kijiji cha Wukiro lakini pia vifaa hivyo vitaenda kukamilisha ukarabati wa nyumba ya mganga kijiji cha Manzeye.
Jumla ya shilingi Milioni 81 zilitolewa na Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini Mhe. Benaya Kapinga kupitia Mfuko wa Jimbo ili kuchochea maendeleo ambapo kati ya fedha hizo jumla ya shilingi Milioni 78.6 zimetumika kugharamia manunuzi ya vifaa hivyo vya ujenzi huku fedha zilizosalia zikielekezwa kwenye manunuzi mengine yatakayohitajika wakati wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenye maeneo husika.
Imeandikwa na Salum Said
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga
Tarehe 3 Februari, 2023
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit