Jumla ya shilingi Milioni 182.5 zimetolewa na Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga kuwezesha vikundi 26 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ndani ya kipindi cha miezi sita kuanzia Julai hadi Desemba 2021/2022.
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Juma Haji Juma mbele ya Mgeni Rasmi Mhe. Aziza Mangosongo Mkuu wa Wilaya ya Mbinga wakati wa hafla ya uzinduzi na kukabidhi hundi za mikopo ya asilimia 10 kwa vikundi 26 iliyofanyika Februari 11, 2022 viwanja vya Parokia, Litembo wilayani Mbinga.
Mkurugenzi huyo ameongeza kuwa pamoja na kiasi hicho cha mikopo kilichotolewa leo, Halmashauri inakamilisha taratibu za mwisho za kutoa fedha nyingine zaidi ya shilingi Milioni 100 kama mikopo ya asilimia 10 kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ndani ya muda mfupi ujao na kwamba matarajio ni kutoa fedha zote za mikopo kwa asilimia 100 ifikapo Juni mwaka huu.
“Kwa sasa ziko zaidi ya Milioni 100 ambazo naamini ndani ya wiki mbili au tatu zijazo tutakua na vikundi vingine tena kwa ajili ya kutoa mikopo; mpaka kufikia Juni kama tutakua tumekusanya kwa asilimia 100, tutatoa mikopo hii ya asilimia 10 pia kwa asilimia 100 ambazo kwa mwaka huu ni zaidi ya shilingi milioni 340”. Amebainisha Mkurugenzi huyo.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Bi. Aziza Mangosongo ambaye alikua Mgeni Rasmi kwenye tukio hilo la kukabidhi hundi amempongeza Mkurugenzi Mtendaji na uongozi mzima wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga kwa kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi CCM, lakini pia kwa mujibu wa sheria, Kanuni na miongozo ya Serikali huku akiwataka wanufaika wa mikopo kutumia fedha hizo kwa malengo yaliyokusudiwa.
“Fedha hizo zina miongo na zinapaswa kurejeshwa kwa mujibu wa mikataba baina ya vikundi na Halmashauri na hatimaye marejesho yatumike kukopesha vikundi vingine”. Bi. Mangosongo ametoa angalizo.
Awali akiwasilisha mwenendo wa utoaji wa mikopo ya asilimi 10 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Bw. Paschal Ndunguru amesema mwaka wa fedha 2020/2021 vikundi 13 vilinufaika na mikopo ya 10% kiasi cha shilingi Milioni 240 zilitolewa na kwamba tayari shilingi Milioni 182.5 zimetolewa kwa vikundi 26 ndani ya miezi sita ya mwanzo kwa mwaka huu wa fedha 2021/2022
Aidha amefafanua kuwa mkakati wa Halmashauri hiyo ni kuchochea ukuaji wa viwanda vidogo na vya kati na kwamba kipaumbele kimewekwa kwenye vikundi vinavyojishughulisha na uchakataji, uokaji, utengenezaji na usindikaji wa bidhaa mbalimbali huku akibainisha baadhi ya faida za mikopo hiyo kuwa ni kuongezeka kwa ajira, mzunguko wa fedha sambamba na kupungua kwa utegemezi ngazi ya familia na jamii.
Imeandikwa na
Salum Said, Mbinga
Tarehe 11 Februari, 2022
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit