Jumla ya wanafunzi 28 kutoka Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Muhukuru (Muhukuru FDC) wamewasili Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ambapo watakua na mafunzo ya vitendo (Field Training) kuhusiana na shughuli za Kilimo na Ufugaji kwa kipindi cha miezi miwili.
Mara baada ya kuripoti kwenye ofisi za Halmashauri zilizopo Kiamili Jumatatu tarehe 6 Machi 2023 wanafunzi hao wamepokelewa na Mkuu wa Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi Mhandisi Evance Haule na kupangiwa vituo vya kazi kwenye maeneo mbalimbali ndani ya Halmashauri hiyo.
Wakiwa Kiamili Mkuu huyo wa Idara alipata wasaa wa kukutana na kuzungumza na wanafunzi katika kikao kifupi ambapo amewakumbusha kutimiza majukumu yao na kuzingatia taratibu wakati wote watakapokua kwenye vituo vyao vya kazi.
Vilevile Mhandisi Haule amesisitiza wanafunzo hao kujikiza katika kutekeleza kile kilichowaleta na kwamba kila mmoja anatakiwa kujiepusha na vitendo vyovyote vya uvunjifu wa amani
Wanafunzi hao wamekumbushwa kutumia weledi na taaluma waliyonayo kikamilifu, kuwa na bidii na ubunifu katika utendaji kazi, lakini kuzingatia maadili na kuhakikisha wanalinda taswira ya Halmashauri, Chuo wanachotoka, familia na jamii zao kwa ujumla.
Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga imekua na utaratibu wa kuwapokea wanafunzi wa kada tofauti kutoka vyuo mbalimbali vya umma na binafsi nchini kwa ajili ya mafunzo ya vitendo na kujitolea kipindi wanapokua likizo na pale wanaposubiri matokeo na ajira mara baada ya kuhitimu masomo yao.
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit