Kamati ya Wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga leo Mei 17, wamefanya ziara ya kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa ndani ya kata ya Kitura, iliyopo Tarafa ya Mbuji ikiwa ni utararatibu wa viongozi hao kutembelea miradi na kusikiliza kero za wananchi Jumatatu ya kila wiki.
Miradi iliyotembelewa na Kamati hiyo ya wataalam iliyongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga, Mwalimu Samwel Komba, ambaye pia ni Afisa Elimu Msingi ni ujenzi wa choo bora cha kisasa (matundu 12) Shule ya Msingi Mzuzu, Zahanati ya Kijiji cha Mahilo, ujenzi wa madarasa mawili na ofisi moja ya walimu Shule ya Msingi Lisau pamoja na jengo la utawala Shule ya Sekondari Kitura, miradi ambayo tayari imeshapelekewa fedha zaidi ya shilingi milioni 50 kwa ajili ya awamu ya kwanza ya utekelezaji wake.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo Mwl. Komba ametoa wito kwa viongozi wa shule, kijiji na kata kuanza mara moja ujenzi wa miradi ambayo tayari fedha zake zimeshatolewa na serikali akitolea mfano ujenzi wa choo cha kisasa shule ya msingi Mzuzu mradi ambao fedha zake kiasi cha shilingi Milioni 13.2 tayari zipo kwenye akaunti ya shule hiyo.
Mwalimu Komba pia amepongeza hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa madarasa shule ya msingi Lisau ambapo amesema kwa hatua iliyofikiwa viongozi waliosimamia mradi huo wameitendea haki fedha ya serikali iliyotolewa na kuwataka viongozi hao na viongozi wengine wote kuwajibika kikamilifu kwa kusimamia vilivyo utekelezaji wa miradi inayotekelezwa kwenye maeneo yao ambapo pia amesisitiza umuhimu wa wananchi kujitolea nguvukazi na kuchangia tofali, mchanga, mbao na vifaa vyote nje ya vile vinavyozalishwa viwandani.
Kaimu Mkurugenzi pia amewataka viongozi wa kijiji na kata kuanza mapema mchakato wa kuandaa madawati huku akionya na kutoa angalizo kwa viongozi kuepuka kuchangisha wanafunzi na wazazi wakati shule zinapofunguliwa ambapo Mwenyekiti wa Kijiji wa Kijiji cha Lisau amemhakikishia Kaimu Mkurugenzi kuwa kwa kuanzia tayari maandalizi ya madawati yameshaanza kwa kupitisha maazimio kupitia mkutano mkuu wa kijiji ya kila kitongoji kuchangia madawati mawili ifikapo Julai 30, 2021.
Kwa upande wao wananchi kupitia kwa Diwani wa Kata ya Kitura, Mhe. Alex Ngui wamemshukuru Mkurugenzi na uongozi mzima wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga kwa kuwapelekea fedha za miradi ya maendeleo na kuomba serikali kuendelea kurahisisha utolewaji wa huduma kwa wananchi kwa kuondoa kero na kupunguza adha ya wananchi mathalani ya kufuata huduma za afya Hospitali ya Litembo kwa wananchi wa Vijiji vya Mahilo na vijiji jirani hasa kipindi cha masika.
Akizungumzia miradi mingi kufikia hatua nzuri ambayo kukamilishwa kwake kuhitaji tu kuwekwa madirisha, dari na kupakwa rangi, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji amemuagiza Kaimu Mhandisi wa Ujenzi, Bw. Hassan Mateleka kuchukua makisio ya kazi na vifaa vyote vinavyohitaji kukamilisha miradi hiyo na kuwasilisha ofisini kwake ili Halmashauri ione namna bora ya kukamilisha miradi hiyo haraka ikiwezakana ndani ya kipindi cha mwaka huu wa fedha 2020/2021 au mwanzoni mwa mwaka ujao wa fedha wa 2021/2021.
Pia Kamati hiyo imetembelea Chama cha Msingi Lisau (Lisau AMCOS) na kukutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa chama hicho cha msingi ambacho kimezaliwa kutoka AMCOS Mama ya Mahilo (Mahilo AMCOS) ambapo viongozi hao wamemthibitishia Kaimu Mkurugenzi na timu yake kuwa chama hicho kinaendelea vizuri na utendaji kazi wake na hakuna mgogogoro wowote baina ya wanachama na viongozi wa kijiji na kata hiyo.
Mwenyekiti wa Lisau Amcos Bw. Batwin Hyera amesema Chama hicho tayari kimeanza kupokea kahawa tangu Mei 5 kuashiria kuanza kwa msimu mpya wa kahawa huku akisema kwa msimu uliopita chama kiliweza kulipa wanachama wake wote kwa bei ya juu ya shilingi 5,200/= kwa kilo na kwamba Amcos hiyo pia imekua ikichangia ujenzi wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa Shule ya Msingi Lisau na Sekondari ya Kitura ikiwemo kuchangia vifaa vya ujenzi na fedha taslimu
Imeandikwa na
Salum Said
Afisa Habari, Mbinga D.C
MBINGA DISTRICT COUNCIL
Sanduku la posta: P.O. BOX 194 MBINGA-RUVUMA
Namba za simu: 2552640005
SImu ya mkononi: PS 0754533018
parua pepe: ded@mbingadc.go.tz
Copyright ©2021 Mbinga District Council. All rights Reserved. Prepared by ICT - Unit